Global Citizen, harakati kubwa zaidi duniani inayopambana kutokomeza umaskini uliokithiri, kwa kushirikiana na Taasisi ya Waislitz, leo imemtangaza Smart Israel, Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa Smartel Agri Tech kutoka Nigeria, kuwa mshindi wa Tuzo Kuu ya Global Citizen Waislitz Prize 2026.

Akikua katika eneo la Middle Belt nchini Nigeria, Smart Israel alishuhudia moja kwa moja jinsi migogoro ya rasilimali, ukimbizi na mabadiliko ya tabianchi vinavyoweza kuchangia njaa na utapiamlo katika jamii yake.

Uzoefu huo ndio uliomhimiza kuanzisha Smartel Agri Tech, kampuni ya teknolojia ya tabianchi inayosaidia jamii zilizo hatarini kutokana na tabianchi kulima chakula chenye virutubisho bila kutumia udongo, katika karibu mazingira yoyote.

Kwa kutumia mifumo ya kisasa ya hydroponic inayoendeshwa na nishati ya jua na kuwezeshwa na Akili Mnemba (AI), Smartel tayari imesambaza zaidi ya mifumo 3,000, na kusaidia maelfu ya wakulima na familia kupata chakula kwa njia endelevu.

Tuzo ya Grand Prize itamwezesha Smart na timu yake kuwafikia kaya 5,000 zaidi kwa uzalishaji wa chakula wa bei nafuu unaohimili mabadiliko ya tabianchi na kupanua mtindo wake bunifu wa vituo vya hydroponic vya jamii.

Kazi ya Smart inaonesha jinsi teknolojia na maarifa ya kienyeji yanavyoweza kuungana ili kujenga usalama wa chakula na ustahimilivu katika jamii zinazokabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchi.

Washindi wengine wa mwaka huu ni Diana Yousef, Mwanzilishi na Mkurugenzi Mtendaji wa change:WATER Labs, aliyepokea Tuzo ya Disruptor Award, na Oghenekevwe William Emadago, Mwanzilishi na Afisa Mkuu wa Uendeshaji wa Girlified LTD, aliyepokea Tuzo ya People’s Choice Award.