
Msanii wa Nigeria, Ekene Ngige, anaendelea kuvutia ulimwengu wa sanaa kwa kugeuza kahawa kuwa rangi yake ya kipekee ya kuchorea. Safari yake ya kiubunifu ilianza mwaka 2016, baada ya kahawa kumwagika kwa bahati mbaya kwenye meza ya mkahawa mmoja jijini Lagos.
Badala ya kuifuta tu, Ngige alivutiwa na madoa ya rangi ya kahawia yaliyobaki, na hapo ndipo wazo la kutumia kahawa kama wino wa sanaa lilipochipuka. Tangu wakati huo, ameachana kabisa na rangi za kawaida na kujikita katika kufanya majaribio na kahawa katika maumbo yake yote.

Kwa umahiri wa hali ya juu, Ngige hutumia kahawa ya unga wa instant, kahawa iliyosagwa, na hata punje nzima za kahawa, akizichanganya kwa ustadi kupata vivuli, muundo na undani wa ajabu. Matokeo yake ni picha za watu zilizo hai na zenye hisia, zinazoonekana kama zimepigwa picha, kazi ambazo zimemletea sifa kubwa ndani na nje ya Nigeria.
Sanaa yake ni ushuhuda wa wazi kuwa ubunifu wa kweli hauna mipaka, na unaweza kuzaliwa kutoka kwenye vitu vya kila siku visivyotarajiwa.



